Sunday, July 1, 2007

KUNA UTAMADUNI MPYA NYUMBANI

Unamkumbuka Rhymson, mmoja wa waasisi wa Hip Hop hapa Tanzania? Alikuwa na kundi la mwanzo kabisa la mtindo huo wa muziki, likiitwa KWANZA UNITY. Siku hizi Rhymson ni mwafrika aliyezaliwa upya na anaitwa Zavara.

Zavara alikuwa ughaibuni kwa takribani miaka isiyopungua kumi, huko Kanada na Marikani. Huko alikuwa akifanya shughuli za mziki pamoja na filamu. Sasa baada ya kipindi chote hicho amerejea hapa nyumbani na kuungana na "Waafrika" wa hapa ili kuweza kupeleka jahazi la mziki wa Hip Hop mbele, katika mstari ulionyooka.

Zavara pamoja na "Waafrika" kadhaa wa hapa akiwemo msanii na mwanaharakti aitwaye Mejah wameungana na kuanzisha mradi uitwao "Uma Project". Huu ni mradi wenye lengo la kukusanya vijana wa "Kiafrika" wenye ndoto ya kufanikiwa katika sanaa bila kuisahau asili yao. Vijana hawa wengi wao ni wale wasio na uwezo wa kifedha kuweza kufanikisha ndoto zao.

Uma Project huandaa tamasha kila jumamosi ya mwisho wa mwezi na kuwakutanisha vijana pale British Council, Dar es Salaam. Sasa jana lilikuwa ni tamasha la tatu na lilipewa jina la "WEWE NI NANI?". Jina hili lina dhumuni la kumfanya kila binadamu kujiuliza kuhusu uwepo wake kabla hujafanya jambo na kuhakikisha iwapo unajitambua. Tamasha la mwezi uliopita liliitwa "USWAZI WAPI?".

Katika tamasha la jana kulikuwa kuna wachoraji, wanamuziki, wapiga picha mgando na za video, watu wa masuala ya mitindo ya mavazi (Wakiongozwa na Merinyo wa Afrika sana), na wengine wengi.

Kila kitu kilikuwa poa sana ila nilivutiwa sana na sanaa ya kuchora grafiti ukutani. Sanaa hii inasimamiwa na kuongozwa na Mejah, yeye ni mtaalamu wa sanaa hii, aliisomea kule New York, Marikani. British Council wamejitolea ukuta ambao vijana wa kitanzania wanapatiwa fursa ya kuandika grafiti kuelezea hisia na mawazo yao. Picha hizi za grafiti hudumu kwa muda wa mwezi mmoja halafu hufutwa na kuta kupakwa rangi nyeupe tayari kwa watu kuchora tena katika tamasha linalofuata.

Elimu ya Grafiti hutolewa bure pale, rangi pia hutolewa bure na jamaa wa British Council. Kwa kweli huu ni utamaduni mpya hapa nyumbani, na ni kitu poa sana kwani unawafanya vijana wa kiafrika kujitambua katika kila wanachijatahidi kufanya.

No comments: